Tuesday, June 18, 2013

CHADEMA UK YAMWANDIKIA BARUA RAISI. PIA YATUMA TAARIFA KWENYE TAASISI ZA KIMATAIFA ZA KUSIMAMIA HAKI ZA BINADAMU, BBC LONDON NA BALOZI MBALI MBALI

TAMKO RASMI CHADEMA UK

CHADEMA UK awali ya yote tunapenda kutoa pole kwa waTanzania na wapenzi wa CHADEMA waliopatwa na kukutwa na janga la kurushwa kwa bomu kwenye mkutano wa CHADEMA wa kuhitimisha shughuli za kampeni za uchaguzi wa madiwani huko Arusha. Tunatuma salam zetu kuwafariji wale wote walioguswa kwa namna moja ama nyingine katika jambo hili.
Kama waTanzania, tunapinga vikali na kukemea kitendo hichi kwa nguvu zetu zote. Mazingira na jinsi kitendo hichi kilivyotekelezwa tuna kila sababu ya kuamini kwamba hili ni tendo la kigaidi. Na kwa sababu hiyo ni jukumu la mamlaka (yaani serikali) na vyombo vyake vya dola kulinda na kuepusha matendo ya kigaidi kama haya.

CHADEMA ni chama kinachoongozwa na watu makini (effective and responsible leaders) wenye kuheshimu mamlaka ya sheria za nchi. Wanachama wa CHADEMA wamekuwa watulivu siku zote wakifuata na kuheshimu sheria kama chama kinavyowaelekeza. Hata pamoja na kwamba yamekuwepo matendo mengi sana yanayoashiria kuukandamiza upinzani (hasa CHADEMA) kwa uwazi kabisa, viongozi wamekuwa mstari wa mbele kuwatuliza wananchi na kuwataka waendelee kuwa na imani na mamlaka. Hii ni dhahiri kwamba imesaidia kuepusha vurugu kusambaa na kuiingiza nchi kwenye balaa la vita baina yetu sisi wenyewe.

Japokuwa chama na hasa sisi wanaCHADEMA UK tutaendelea kutafuta mbinu nyingine katika kupambana na uonevu huu kwa njia ya amani (baadhi kama tulivyoanisha hapo chini), tunapenda pia kuitahadharisha mamlaka kutokujisahau (against complacency) kwamba kama hatua za msingi hazitachukuliwa uvumilivu wa waTanzania utafikia kikomo. Hili ni KARIPIO KALI kwa mamlaka zinazohusika na kwa sababu hiyo tumechukua hatua zifuatazo:
1.    Tumetuma barua ya rasmi ya ushauri kwa kwa Raisi wa Jamhuri ya Muungano mh. J.M Kikwete. Pamoja na mambo mengine tumetoa maoni yetu kama ifuatavyo:
Usalama wa taifa ufanyiwe marekebisho makubwa: Tanzania Intelligence Services (TIS) inahitaji kufanyiwa marekebisho na ikibidi ivunjwe na kuwe na vikosi vifuatavyo:
o    Tanzania Secret Intelligence Services (TSIS): Hii iwe ni mamlaka ya kutafuata, kupata na kusimamia siri za kimataifa ikiwa ni katika kulinda nchi na mipaka yake. Kwa kushirikiana na vyombo mbali mbali TSIS itakuwa na jukumu la kupata siri za kijeshi, ugaidi wa kimataifa, n.k.
o    Tanzania Serious Organised Crime Unit (TSOCU): Kitengo hiki kiwe na wajuzi wa maswala mbali mbali ikiwahusisha Polisi maalumu, wataalamu wa computer na mawasiliano, na wajuzi wenye uelewa wa kuchunguza matendo ya kijangili. Kazi kubwa ya kitengo hiki iwe ni kuchunguza na kuwakamata wahalifu wote wanaofanya matendo ya kijangili ikiwa ni pamoja na madawa ya kulevya; wizi ndani ya mashirika na taasisi za serikali unaofanywa na kupangwa na wafanyakazi kwa kushirikiana na watu mbali mbali; Mauaji; n.k. Hata hivyo kazi nyingine muhimu ya TSOCU iwe ni, kwa kutumia njia za kisasa kabisa, kugundua mapema na kuzuia uhalifu kutokea. Kama wakipatikana wana usalama wenye uwezo, kitengo hiki kitaepusha upotevu wa maisha ya watu wasio na hatia kwa kiwango cha juu. Cha muhimu ni kuhakikisha kitengo hiki kinapatiwa vifaa na mafunzo ya kisasa kabisa ili kufanya kazi zake kwa ufanisi zaidi.
Kuna umuhimu mkubwa sana wa kuvipa uhuru vyombo hivi vya usalama kutoka kwa wansiasa. Kwa mfano ilivyo sasa wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa ndiyo wenyeviti wa kamati za usalama za wilaya na mikoa. Hivi vyote ni vyeo (appointement) vya kisiasa. Kwa hivyo kama CHADEMA hatuamini kabisa kwamba vyombo hivi vinaweza kusimamia maswala ya kiusalama kwa haki bila upendeleo wa kisiasa.
Kazi za jeshi la polisi ziwe za kufanya kazi karibu kabisa na wananchi katika kusimamia sheria, kulinda wananchi na mali zao, kuzuia uhalifu, na kuwapunguzia wananchi hofu ya kufanyiwa vitendo vya kihalifu ili kumfanya kila mwananchi ajisikie huru. Hii itakuwa ni kuhakikisha jamii inaishi kwa kufuata sheria na taratibu (maintaining public order), kupambana na wahalifu na kwa kushirikiana na vyombo vingine vya usalama.

Hata hivyo jeshi hilo linahitaji kufanyiwa mabadiliko makubwa. Dosari kubwa zinaonekana dhahiri kuanzia kwenye ngazi za mkuu wa jeshi hilo nchini (IGP), kwenda chini kwenye ngazi za wakuu wa polisi wa mikoa (RPCs), wakuu wa vitu (OCSs) na polisi wa kawaida. Kwa mfano mauaji yanapotokea, hakuna uwajibikaji (accountability).
Kwa sababu hiyo kuna umuhimu wa kuzipa nguvu kamati ya ulinzi na usalama ya bunge ili ziweze kuwaita na kuwahoji wakuu wa usalama ili wajieleze mbele ya kamati pale inapohitajika.
2.    Tumeandika barua kwenda kwenye ofisi za haki za binadamu (International Human Rights Office) hapa London. Nia na madhumuni ni kuwapa picha ya vitendo vya kinyama vinavyofanywa na baadhi ya watu kwa manufaa yao binafsi.
3.    Tumetuma barua kwenye balozi zaidi ya nane za nchi mbali mbali tukiyaeleza na kuyaanisha matukio yanayoendelea ndani ya nchi huku viongozi wetu wakikaa kimya.
4.    Tumevitaarifu vyombo mbali mbali vya habari kama vile BBC, RT Television na Aljazeer kuhusu hali na mwelekeo wa kisiasa Tanzania ambao umeanza kuchukua sura mpya.
Kwa nguvu zote tutaendelea kuueleza ulimwengu na kukaripia uhalifu huu tunaofanyiwa ndani ya nchi. Ni muhimu kwa waTanzania kufahamu kwamba upinzani siyo dhambi . Upinzani ni mawazo mbadala.

Kwa wana-CHADEMA wenzetu
Tanzania ni nchi yetu tunayoipenda na kuithamini. Tunaamini kabisa kwamba amani na utulivu ni vitu muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu. Sote tunatamani kuwarithisha watoto wetu (next generation) nchi itakayowapa fursa ya kusonga mbele. Hata hivyo amani tunayoiongelea hapa si amani ambayo tumeaminishwa na serikali ya ccm kwa miaka mingi. Amani tunayoisema ni amani ya kweli, amani inayoheshimu utu, amani inayompa fursa kila mwananchi kufanya shuughuli zake bila kuogopa ili mradi anafuata sheria za nchi.
Ni dhahiri kwamba wengi tumechoshwa na uongozi mbovu ambao tumeifikisha nchi hii hapa tulipo leo. Wengine hata tunashangaa kwamba hawa hawa ambao wamekuwa madarakani kwa miaka zaidi ya 50 bila kuleta maendeleo yeyote, leo hii wanaonekana kutaka kung’ang’ania madaraka kwa gharama zozote zile hata kwa kumwaga damu. Watu hawa wanaonesha uchu na jazba ya hali ya juu lakini wakiambiwa wajieleze ni nini wamekifanya kwa miaka 50 hawana jibu. Ikiwa kama haitoshi, wengi tunaona kwamba sasa imetosha, tumeshavumilia vya kutosha (enough is enough).
Pamoja na hayo tunawaomba wanaCHADEMA wote kuendelee kutetea bila kuchoka juhudi za kulikomboa taifa letu. Juhudi hizi zitazaa matunda siku siyo nyingi.
Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Nchi Yetu

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...